Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Tuesday, October 14, 2014

'HATUITAKI KATIBA MPYA PENDEKEZWA'


CHAMA cha Wananchi (CUF) kimesema hakiikubali Katiba inayopendekezwa kwa kuwa haina maslahi ya wananchi wa Zanzibar.
Badala yake chama hicho kimewataka Wazanzibari waikatae Katiba iliyopendekezwa na Bunge Maalum la Katiba (BMK).
Kauli hiyo ilitolewa jana na Katibu Mkuu wa CUF ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad, wakati akihutubia mkutano mkubwa wa hadhara katika viwanja vya Demokrasia vya Kibanda Maiti, mjini Zanzibar.
“Wananchi, Katiba haikubaliki kwa Wazanzibari, mimi mwenzenu siikubali, sijui nyinyi wenzangu?” alihoji Maalim Seif na wananchi kuitikia kuwa nao hawaikubali.
Alisema kuwa miongoni mwa mambo yanayoipokonya Zanzibar hadhi yake ni Katiba inayopendekezwa kumpokonya Rais wa Zanzibar mamlaka ya kugawa mikoa, tofauti na Katiba ya Zanzibar ya sasa. 
Alisema kwa maana hiyo Rais wa Muungano anachukua mamlaka ya Rais wa Zanzibar na anaweza kuteuliwa wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya wa Zanzibar. 
“Kwa mabadiliko hayo ya rasimu ya Chenge, Rais wa Muungano anaweza kututeulia Sheha wa Shehia ya Mtoni Zanzibar kutoka Bukoba,” alisema Maalim Seif huku akishangiliwa na wanachama na wafuasi wa CUF.
Maalim Seif alisema Katiba ya Zanzibar na marekebisho yake ya mwaka 2010 iko sahihi kabisa na inazingatia matakwa ya Makubaliano ya Muungano.
Alisema hayuko tayari kuona rasimu hiyo inakubalika na kwamba Wazanzibari hawataki kuiona.
Alisema hakubaliani na kauli za baadhi ya watu waliosema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) inaridhishwa na mchakato wa Katiba mpya.
“Nataka kuwambia hakuna kikao chochote cha SMZ kilichokaa na kusema tunaijadili rasimu, kama kuna mtu anataka kusema eti Smz imeridhishwa aseme mwenyewe binafsi na siyo Serikali ya Umoja wa Kitaifa,” alisema Maalim Seif.
Maalim Seif aliisifu Rasimu ya Jaji Joseph Warioba ambayo ndiyo ilizingatia matakwa ya Watanzania walio wengi na kwamba pamoja na awali Wazanzibari kupendekeza muundo wa Muungano wa mkataba, lakini kwa busara ya tume hiyo waliikubali muundo wa serikali tatu.
Maalim Seif alisema anahutubia mkutano huo akiwa na furaha kubwa kutokana na umma ulioteremka katika viwanja vya Kibandamaiti, na hiyo ni sababu tosha na ujumbe kuwa hawaitaki Katiba inayopendekezwa.
“Ndugu yangu, rafiki yangu Rais Jakaya Kikwete ufahamu kuwa umma huu uliohudhuria Kibandamaiti ni ujumbe tosha kuwa Katiba hiyo hawaitaki, na mwambia Rais Kikwete kuwa Katiba hii hatuikubali,” alisema Maalim Seif. 
Maalim Seif alisema Katiba bora ni ile inayozingatia maoni ya wananchi. 
“Lakini Rais (Rais Jakaya Kikwete), Katiba yenu mmeweka upande maoni ya wananchi, mmejifungia wenyewe, mmeipitisha wenyewe na mmeichezea ngoma wenyewe”, alisema. 
Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Nassor Ahmed Mazrui, alisema wajumbe saba wa Bunge Maalum la Katiba waliopiga kura ya Hapana hadharani kukataa rasimu hiyo ni mashujaa wa Zanzibar na Wazanzibari wote wanapaswa kuwapa heshima kubwa.
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa CUF, Salum Bimani, alisema wananchi wa Zanzibar wameshaamua na hawatarejea nyuma zaidi ya kuiondoa CCM mwaka 2015 na kuipa Zanzibar mamlaka kamili.
Bimani alisema msiwape kura viongozi wa CCM ambao wanauza nchi ya Zanzibar huku wakicheza ngoma.
“Kwa Shilingi 300,000 watu hawa wanadiriki kuuza nchi, hawa waliopiga kura za ndiyo ni madalali wa Zanzibar, hata wale waliopiga kura za siri pia ni madalali,” alisema Bimani.
Alisema wanasheria wawili wameitetea Zanzibar na wakafikwa na masahiba mazito.
Aliwataka wanasheria hao kuwa Jaji Walfgong Dourado na Mwanasheria Mkuu wa Serikali aliyefutwa kazi, Masoud Othman Masoud.
Bimani alisema Wazanzibari wapo pamoja nao katika kuhakikisha Zanzibar inabaki na wale wenye nia mbaya wajue kwamba Zanzibar wataitapika watake wasitake. 
Mansour alisema naendelea kuwa muumini wa Maridhiano ya Zanzibar. Katiba hii ni yao wenyewe si ya Wazanzibari.
“Baada ya kuona umma huu uliohudhuria katika mkutano huu tunapaswa kumhofia Mwenyezi Mungu,” alisema.
“Naendelea kumuunga mkono Maalim Seif Sharif Hamad, ni kiongozi asiyekuwa mnafiki anajitambua na hatawaliwi na utawala wa Dodoma, anatawaliwa na Wazanzibari wenyewe na matakwa na matumaini yao,” alisema na kuwataka Wazanzibari wasiwe na hofu kwani hawawezi kufungwa wote wako wengi sana, wakati umefika. 
“Tumeungana kwa hiari yetu, tukakubali kwa hiari yetu, sisi si watumwa wa mtu yoyote, tumefungwa tumefukuzwa makazini kwa sababu ya nchi hii, hatuwezi kurudi nyuma,” alisema.
Alieleza kuwa watu wasishangae kumuona Mwenyekiti wa Kamati ya Maridhiano, Mzee Nassoro Moyo, amesimama kwenye jukwa anatetea nchi yake.
Mzee Moyo alisema Wazanzibari hawakubalini kuona watu wanataka kuichukua nchi yao ovyo ovyo.
Mkutano huo ambao ni wa kwanza kuhutubia na Maalim Seif tangu BMK limalize kazi yake na kuwasilisha rasimu kwa Rais Jakaya Kikwete na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, ulihudhuriwa na maelefu ya wananchi huku baadhi yao wakibeba mabango.
Baadhi ya mabango hayo yalibeba ujumbe usemao “Wapige mabomu rasimu yao hatuitaki, Hongera Othman Masoud, Katiba ya vijisenti (Chenge) hatuitaki”. 
Katika hatua nyingine, Maalim Seif alikanusha taarifa kwenye mitandao kuwa hatajiuzulu wadhifa huo na ataendelea kukiongoza CUF kushika madaraka na kushika Serikali ya Umoja wa Kitaifa katika uchaguzi mkuu wa mwakani, akiwa kwenye nafasi hiyo.
Maalim alisema taarifa zilizoenezwa kwenye mitandao ya kijamii kuwa baada ya kufukuzwa Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Masoud Othman Masoud, naye amejiuzulu Umakamu wa Kwanza ni uzushi mtupu.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...